Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This
 
MAHAKAMA ya Wilaya ya Kibondo Mkoani Kigoma, imewapa adhabu ya kufua mashuka ya hospitali na kusafisha mitaro ya barabara kwa muda wa siku 14, watu wanne akiwemo Diwani wa Kata ya Kasanda Wilayni Kakonko kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), baada ya kukutwa na hatia ya makosa matatu.
Mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Kibondo, Erick Marley, Mwendesha Mashitaka wa Polisi Peter Makala, amemtaja diwani huyo kuwa ni Dicksoni Barutwa (40), na Daudi Obadia (32), Hatari Kasase (33) na Brighton Jonas (29), wote wakazi wa Kata ya Kasanda wilayani Kakonko.
Makala alisema kuwa Novemba 8 mwaka jana -2014 majira ya saa kumi jioni katika Kijiji cha Kazilamihunda, watuhumiwa wote kwa pamoja walifika eneo la Ofisi ya Mtendaji wa Kijiji hicho isivyo halali kisha kuifunga Ofisi hiyo kwa kuweka gundi aina ya Super Grew, na unga wa ngano kwenye kufuri ili kuzuia mtendaji asifanye kazi yake.
Inadaiwa kuwa watu hao walifikia uamuzi huo kwa madai kuwa hawamtaki Mtendaji huyo wa kijiji Amosi Peter, na kumtishia kuwa watamuua.
Kufuatia hali hiyo Diwani huyo na wenzake, mahakama ya Wilaya ya Kibondo, imewahukumu kulipa faini ya shilingi elfu 50 au kufungwa jela miezi mitano kwa kosa la kufunga Ofisi ya Mtendaji na pia kulipa faini ya shilingi elfu 50 au kutumikia jela miezi miwili kwa kosa la kufanya fujo.
Watuhumiwa wote wamelipa faini hizo na kuachiwa huru isipokuwa Hatari Kasase (33), ambaye anakabiliwa na kesi nyingine ya mauaji hivyo anaendelea kusalia gerezani.
Aidha katika kosa la kutishia kuua diwani Barutwa, na wenzake wamehukumiwa adhabu ya kazi za kijamii ambayo ni kufua mashuka ya hospitali ya wilaya ya kakonko kwa muda wa wiki moja na kuzibua mitaro ya barabara kwa muda wa wiki moja ambapo tayari wamekabidhiwa katika Idara ya Maendeleo ya Jamii, na wataanza kutumikia adhabu hiyo baada ya siku kuu ya Pasaka.
Watuhumiwa wengine katika kesi hiyo ambao ni Boniface Obadia (35), Amos Buseni (33), Majaliwa Charles (24), pamoja na Samora Barichako (35), wote wakazi wa kijiji Cha Kazilamihunda wilayani Kakonko wameachiliwa huru baada ya kukutwa hawana hatia katika mashauri yote.
Chanzo:Kigomalive

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top