TAARIFA YA WAJUMBE WA BARAZA KUU NA MKUTANO MKUU WA CHADEMA KWA UMMA.
A. UTANGULIZI
Ndugu wanahabari.
Mbele yenu
ni viongozi halali wa chama cha demokrasia na maendeleo CHADEMA kutoka
mikoa yote ya Tanzania kwa uchache tumekutana jumla ya wajumbe 78
kuwakilisha wenzetu walioshindwa kufika kwa sababu mbali Sisi
ni wajumbe wa Baraza Kuu na mkutano mkuu wa Chama ambapo pamoja nasi
tumejumuika na wenyeviti wa mabaraza ya WANAWAKE WA MIKOA YA TABORA NA
SINGIDA, MWENYEKITI WA VIJANA MKOA WA TABORA pamoja na MUASISI WA
CHADEMA kutokea mkoa wa SINGIDA na mwenyekiti wa M4C wilaya ya SINGIDA
hivyo tunafanya jumla ya tuliokutana kwa jambo hili kuwa ni wanachadema
82.
Tumewaita
kuwaeleza namna ambavyo tumekuwa tukisononeshwa na mwenendo wa chama
chetu kwa kipindi kirefu sasa, hivyo tunaomba mtusaidie kuufikishia umma
mawazo ya wanachadema tunaowawakilisha huko mikoani tutokapo.
B. KUSHINDWA KWA UONGOZI WA KITAIFA.
Tunasikitika kuona kwamba kadri siku zinavyoenda Uongozi wa juu wa chama unazidi kushindwa kufanya kazi ya kukiimarisha chama.
Baada ya
jitihada tulizozifanya kwenye uchaguzi wa 2010 sehemu mbali mbali, ni
dhahiri ushindani kwa sasa ungekuwa mkubwa sana kiasi cha chama kushika
dola uchaguzi ujao iwapo chama kingejikita kwenye jitihada za ujenzi wa
chama.
Badala yake
uongozi wetu umewasaliti Watanzania waliokuwa na tumaini kubwa sana na
chadema na kuwekeza nguvu nyingi sana kwenye Kuimarisha migogoro baina
ya viongozi wakuu wenyewe kwa wenyewe, wanaimarisha ubinafsi miongoni
mwa wanachama, wanaimarisha Udini na Ukabila pamoja na ubadhilifu wa
mali za chama.
Matendo haya
ya viongozi wetu ni UNAFIKI wa kisiasa, kiasi cha kutumia mabilioni ya
shilingi kwenda kumshambulia ama kummaliza kisiasa kiongozi mwenzao
(Zitto Kabwe) na kuacha ujenzi wa chama ukiendelea kuporomoka.
Kwenye
ujinga huu, hakuna wa kumlaumu zaidi ya Mwenyekiti wetu Freeman Mbowe na
na Katibu Mkuu Dkt.Wilbrod Slaa. Hawa wanafaa sasa kuhukumiwa na
watanzania wanaopenda mabadiliko ya kweli kwa kurudisha nyuma jitihada
za kuwakomboa na kukiimarisha chama na badala yake wamekuwa wakitumia
nguvu kubwa na rasilimali nyingi za chama kujiimarisha wao wenyewe.
C. UBADHILIFU WA FEDHA NA MALI ZA CHAMA.
Ndugu WanaHabari.
Mtakumbuka
kwamba baada ya uchaguzi wa mkuu wa mwaka 2010 ruzuku ya chama
iliongezeka kutoka million 56 mpaka milioni 239 kwa mwezi.
Tunasikitika
kuona kwamba mpaka sasa chama kimeshindwa kufanya uwekezaji wenye tija
ili kukisaidia chama kiweze kujiendesha bila kutegemea Ruzuku ama kukopa
kutoka kwa Mbowe kama mwenyewe anavyopenda tuwe tunafanya.
Mpaka sasa
chama kimepokea jumla ya shilingi BILIONI 10.038 kama ruzuku kutoka
serikalini ili chama kijiendeshe. Ni narudia, mpaka sasa chama kimepokea
kutoka serikalini jumla ya SHILINGI BILLION KUMI, NA MILIONI THELASINI
NA NANE.
Cha
kusikitisha kwa kipindi chote hicho na kiasi chote hicho cha pesa
zitokanazo na kodi za waTatanzania pesa ambazo zinasababishwa na kazi
kubwa tuliyoifanya ya kukipigania chama kwenye uchaguzi mkuu wa 2010,
leo chama hakina hata jengo moja la OFISI MIKOANI KOTE na OFISI zote za
mikoa tunapanga kwenye FREMU za maduka na hata Pango la fremu hizo
tunajilipia wenyewe kwa kuchangishana, Mbowe na Slaa wanatumia MABILIONI
HAYA KURUKA NA CHOPA sisi huku chini tunaendelea kumenyeka kwa kigezo
cha UKAMANDA ,huu ni utumiaji mbaya wa mali za chama.
Tunasikitishwa
sana na kitendo cham mwenyekiti MBOWE kusema anajilipa madeni
aliyokikopesha chama kila siku, kiasi cha zaidi ya MILLIONI 700 Mbowe
anajilipa kama madeni aliyokikopesha chama. Sasa tunashindwa kuelewa
deni hili ni deni gani lisiloisha?, na je deni hili alikikopesha chama
kwa mkataba gani?, na aliusaini mbele ya nani huo mkataba wa mkopo?,
Taratibu za chama kukopa zipo wazi je zilifuatwa?. Haya ni matumizi
mabaya ya fedha za umma.
Tunasikitishwa
na kitendo cha mwenyekiti mbowe kukiuzia chama MAGARI CHAKAVU kwa zaidi
ya million 600, Huku akijua ni chakavu na kwamba kabla ya kukiuzia
chama alikuwa anakikodisha magari hayo
Masikitiko
yetu ni kitendo cha MBOWE kununua LANDCRUISER V8 VX 2 kwa pesa za chama
na kasha kuja kukiuzia chama, lakini kama haitoshi mpaka leo hii Gari
hizo zimesajiriwa kwa majina ya MBOWE HOTELS. Haya ni matumizi mabovu
mno ya mali za umma na kwamba yampasa sasa ajitathmini kama anapaswa
kuendelea kuwa kiongozi mtetezi wa wanyonge ama mnyonyaji wa wanyonge.
Tunahudhunishwa
na kitendo cha Dkt. SLAA kutufanyia huduma ya kutuuzia ukombozi,
haiwezekani kwa akili ya kawaida, ukawa katibu mkuu unayelipwa zaidi ya
million 130 kwa mwaka na chama halafu makatibu na viongozi wako wa
mikoani wanalipwa 0 kwa mwaka. Huu ni udalali na unafiki wa kisiasa.
D. UVUNJIFU WA KATIBA NA KANUNI ZA CHAMA.
Mpaka sasa viongozi wakuu hawa, wamevunja katiba ya chama kwa mambo makuu matatu yafuatayo.
1. Kitendo cha kutoka na kususia kwenye Bunge la katiba bila kuruhusiwa na vikao halali vya chama.
Bunge la katiba lilikuwa ni mazao ya Juhudi zetu sisi wanaCHADEMA tuliopambana nchi nzima kuidai katiba.
Chama chetu
kilikuwa na fursa kubwa ya kutuwakilisha kwenye kuandika katiba hiyo na
kufanya marekebisho makubwa kwa kadri tulivyoazimia.
Lakini
kususa Bunge la katiba lililotokana na Sheria mliyoishiriki kuitunga, ni
kutufanya sisi sote tunaowakilishwa na viongozi hawa tuonekane ni
majuha.
Kwa kuwa
CHADEMA ni miongoni mwa waasisi wa mchakato huu wa Katiba. Ni kuwasaliti
Watanzania na kuikosesha nchi fursa ya kuandika katiba kususa.
2. Kitendo cha Kuunda Baraza Kivuli la mseto na vyama tulivyowaaminisha watanzania kuwa vina ushirika na CCM.
Kwenye hili,
chama kinapaswa kuelezwa kama mazingira yaliyowafanya wenzetu hawa
kuungana na CCM yamebadilika ama bado yapo?, Chama kinapaswa kuelezwa na
mbowe na Slaa kuwa Uteuzi wa Mbatia kuwa Mbunge wa kuteuliwa na Rais wa
CCM umebatilishwa ama la?.
Lakini chama
pia kitueleze kama Nafasi ya juu ya viongozi wa CUF kwenye serikali ya
mseto na CCM kule Zanzibar haipo tena. Vinginevyo viongozi wetu wote
walioshiriki hili wanatakiwa wawajibike haraka iwezekanavyo.
3.
Kutokuitishwa kwa mkutano wa Baraza Kuu. Katiba yetu inatuagiza Kuwa
Baraza kuu la chama litaitishwa kila baada ya miezi kumi na mbili. Kwa
kuwa baraza kuu la mwisho liliitishwa February 2013, kulipaswa kuitishwa
tena baraza kuu lingine kabla ya mwezi February 2014 kuisha.
E. AGIZO
- Tunawaagiza viongozi wetu waitishe haraka MKUTANO WA BARAZA KUU ili pamoja na mambo mengine viongozi wetu wajieleze mbele ya Wajumbe ni kwanini Tusiwachukulie hatua za kinidhamu kwa makosa ya UBADHILIFU, KUSALITI NDOTO ZA WATANZANIA, na KUHAMASISHA MGAWANYIKO NA UBAGUZI NDANI YA CHAMA.
- MBOWE na Dkt. SLAA wanatakiwa wajipime wenyewe kama ni sahihi chama kukodi HELKOPTA (CHOPA) 3 na kutumia zaidi ya BILIONI 1.4 za ruzuku ambazo ni kodi za Watanzania halafu eti tunashinda KATA TATU kati ya zaidi ya KATA 27, Yaani kila HELKOPTA MOJA imeleta KATA MOJA ama kila SHILINGI MILLIONI 466.6 kwa KATA MOJA, halafu chama hakionyeshi kushtuka wala Kujali
- MBOWE na Dkt. SLAA wajipime zaidi kama wanafaa kuendelea kuwa viongozi wa chama huku chama kikizidi kudidimia kila uchao kiasi cha KUDHARIRISHWA KWA kupata KURA 2000 CHALINZE na KURA 5000 KALENGA huku chama kikitumia zaidi ya MILLIONI 600 kushiriki CHAGUZI HIZO.
N:B. ORODHA YA WAJUMBE WALIASHIRIKI IMEAMBATANISHWA
Imesomwa leo 23.6.2014 kwa niaba ya wajumbe nami;-
ATHUMANI H. BALOZI
…………………………..
0756767672
KATIBU WA CHADEMA MKOA WA TABORA
MJUMBE BARAZA LA MASHAURIANO KANDA YA MAGHARIBI
MJUMBE WA MKUTANO MKUU CHADEMA TAIFA.
Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro









Post a Comment
Post a Comment