Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Ali Hassan Ali, Msomali anayeishi katika kambi kubwa ya Dadaab huko kaskazini mashariki mwa Kenya, amesema anahuzunishwa na kujiua kulikotokea hivi karibuni kwa rafiki yake Mwethiopia na mwanakambi mwenziye wa muda mrefu.

Kijana mdogo wa Kisomali aliyechafuka vumbi usoni akisubiri pamoja na wakimbizi wengine kwenye kituo cha usajili katika kambi kubwa ya wakimbizi ya Dadaab Agosti 2011. Hali ngumu ya maisha katika makambi na msongo sugu umesababisha baadhi ya wakimbizi kujiua. [Tony Karumba/AFP]

Kila siku kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, Ali, mwenye umri wa miaka 35, alisema yeye na rafiki yake Abdi Aden Hussein walikuwa wakienda pamoja kila siku kuangalia mbao za matangazo zinaorodhesha majina ya wakimbizi walioidhinishwa kwa upataji wa makazi mapya.

Wanaume hao wawili walikuwa na hakika kwamba siku moja maombi yao ya upataji wa makazi mapya yatafikiwa, Ali alisema, lakini maombi ya Hussein yalikataliwa kabisa.

"Tulituma maombi pamoja kwa ajili ya upataji wa makazi mapya. Huku nikisubiri kupata makazi mapya huko Marekani, Abdi hakufanikiwa," aliiambia Sabahi.

Tarehe 9 Juni, Hussein, mwenye umri wa miaka 34, alijiua katika kambi ya Ifo I ya Daadab, Ali alisema.

Mahema yamejaa katika viunga vya kambi ya wakimbizi ya Dagahaley katika kambi kubwa ya wakimbizi ya Dadaab huko Kenya Julai 2011, katikati ya ukame na njaa inayoua ambayo iliwalazimisha Wasomali wanaokadiriwa 1,300 kila siku kuomba hifadhi nchini Kenya, kwa mujibu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa. [Phil Moore/AFP]

Wale waliongizwa katika orodha fupi kwa usaili kwa kawaida huwa na furaha sana kwa sababu maombi yao kwa ajili ya upataji wa makazi mapya kwa hakika yanahakikishwa, Ali alisema, lakini waombaji wanaokosa hutafuta njia ya mkato kwa kuharibikiwa na kwamba wanazamisha huzuni zao kwenye madawa ya kulevya au kujiua wenyewe.

Osman Yusuf Ahmed, mkimbizi wa Kisomali mwenye umri wa miaka 39 ambaye ameishi katika kambi ya Hagadera kwa miaka 17, aliiambia Sabahi kwamba kaka yake Musa alijiua mwezi Disemba baada ya maombi yake kadhaa ya kupewa makazi mapya kutofanikiwa.


"Alikuwa na shauku kubwa na maisha ya Ulaya kwa sababu ya hadithi za mafanikio ambazo zinavutia katika makambi," Ahmed aliiambia Sabahi.

"Baada ya maombi ambayo hayakufanikiwa, alijitenga. Katika matukio ya nyuma aliniambia kwamba maisha hayana maana, lakini niliendelea kumtia moyo kwamba haukuwa mwisho wa kila kitu," Ahmed alisema, lakini hakukuwa na mafanikio.

Yusuf Ali Elmi, Msomali mwenye umri wa miaka 33 ambaye ameishi katika makambi ya wakimbizi nchini Kenya tangu 1995, alisema mara kwa mara alifikiria kujiua kabla ya hatimaye kuwa na sifa ya kupata makazi mapya Marekani mwezi Mei.

"Mawazo ya kukata tamaa yana nguvu unapokuwa pekee yako au unapokosa mwelekeo," Elmi aliiambia Sabahi. Kuelezana aliyoyapitia na hisia zake na wengine ndiko kulikomfanya asubiri kwa muda mrefu, alisema.

Licha ya kushindwa kupata makazi mapya, wakimbizi wengi wanakabiliwa na msongo mkubwa kutokana na hali duni ya maisha na changamoto za maisha katika kambi zilizojaa, ambazo zinawasababishia baadhi kujiua, alisema.

Idadi ya waliojiua haijulikani
Jitihada za kupata takwimu rasmi za idadi ya waliojiua katika kambi za wakimbizi Kenya hazikufanikiwa. Viongozi kutoka Shirika la Kimataifa la Uhamiaji walikataa kujibu maombi ya mahojiano.

Ofisa wa Wilaya ya Dadaab Bernard ole Kipury alikiri kwamba kujiua kumetokea katika kambi, lakini katika matukio kadhaa, sababu ya kifo bado haijulikani, alisema.

"Jamii ya wakimbizi iko katika tahadhari, na hata ambapo kujiua kuliko wazi kunafanywa, wanafamilia wanasisitiza kwamba kichukuliwe kama kifo cha kawaida," aliiambia Sabahi.

"Waathirika wengi wanazikwa hata kabla mamlaka hazijafahamishwa. Tunapata taarifa muda mrefu baada ya mazishi kufanyika, wakati hatuna lolote la kufanya," alisema.

Kuzuia tatizo la kujiua katika kambi ya Dadaab na kambi nyingine na kusaidia wakimbizi kukabiliana na hisia zao, mashirika ya wakimbizi yanapaswa kuingiza huduma za ushauri wa kisaikolojia katika programu zao, alisema Edward M'Mutungi, mhadhiri wa muda wa saikolojia katika Chuo Kikuu cha Daystar mjini Nairobi.

"Wakati wakimbizi wanapowasili na wakati wanaishi katika kambi, wanapaswa kuhakikishiwa kwamba kila kitu kitakuwa sawa na kupewa hisia za matumaini," aliiambia Sabahi.

"Kila mmoja, ikiwa ni pamoja na wakimbizi, wanataka maisha mazuri. Mkimbizi ambaye wakati wote amekuwa akifikiria vita nyumbani na siku zijazo utasababisha madhara wa kimwili na akili. Ushauri unaweza kufanyika katika vikundi au kwa mtu mmojammoja," alisema.

Kukabiliana na tabia ya mauaji, wakimbizi wenyewe wameshauriana aina isiyo rasmi ya tiba ya vikundi, alisema Moulid Ali Hassan, mkimbizi wa Somalia mwenye umri wa miaka 35 katika kambi ya Ifo.

Wakimbizi wameanzisha michezo mbalimbali ya pamoja kambini, ambayo wameipa jina la utani la "kona za msongo", alisema. Wakimbizi wasiofadhaika hukutana hapo kutoa matatizo yao miongoni mwao wenyewe.

Wanaweza kukutana kuanzia alfajiri hadi jioni wakizungumza kuhusu mada mbalimbali ikiwa ni pamoja na fursa za kazi kambini, siasa nchini Somalia, matarajio ya kupata makazi mapya, matatizo katika ndoa zao au ukiwa, alisema.

"Katika kona za msongo, mtu anaruhusiwa kuzungumza kwa sauti ya juu, kunong'ona, kugumia, kulaani, kuwia, kutapatapa, kuapa na kulia. Tunawafariji na kuwanasihi kila mmoja," aliiambia Sabahi.

"Mwishoni, mtu huondoka mahali hapo akijisikia kwamba ameondoa baadhi ya machungu," alisema.

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top