Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Wakati al-Shabaab walipotawala zaidi ya nusu ya Somalia kwa miaka kadhaa, wazazi wengi wa Somalia walilazimishwa kufanya mipango kwa ajili ya watoto wao wa kike kutoroka kulazimishwa kuolewa na wapiganaji wa kikundi cha wanamgambo hao.

Wanawake wa Somalia wakitembea ndani ya kambi ya wakimbizi ya Dolo Ado huko mashariki mwa Ethiopia. Wanawake wengi walitoroka Somalia kwenda nchi jirani kuepuka ndoa za kulazimishwa na wanamgambo wa al-Shabaab. [Judith Schuler/World Food Programme/AFP]

Wanawake hawa walitorokea Kenya, Uganda na Ethiopia, lakini sasa wameanza kurejea nyumbani kadri vikosi vya Somalia na Misheni ya Umoja wa Afrika nchini Somalia (AMISOM) vinavyochukua udhibiti wa maeneo mengi kutoka kwa al-Shabaab..

Jijini Mogadishu, Liban Ahmed alikumbuka namna mmoja wa mabinti zake watatu alivyolazimishwa kuolewa na mwanachama wa al-Shabaab mwaka 2009.

"Binti yangu alikuwa mdogo sana na hakuwa na utashi wa ndoa wakati mwanachama huyo asiye mwema alimuoa kwa lazima," alisema Ahmed, mwenye umri wa mika 45. "Alikuwa na miaka 16 na alikuwa shule darasa la saba."

"Mwanaume ambaye hakuwa ananijua mimi wala familia yangu alikuja nyumbani, akiwa na silaha aina ya AK-47," Ahmed aliiambia Sabahi. "Aliniambia, 'Ninataka kumuoa binti yako Zamzam na mimi ni mpiganaji wa vita vitakatifu Abu Akram.' Nilimwita binti yangu kwa haraka na kumuuliza kama alikuwa akimjua mwanaume huyo, lakini alipomwangalia hakuweza kumtambua, jambo lililotutisha sote," alisema.

Ahmed alisema kuwa alihisi kutishwa lakini hata hivyo alimwambia mvamizi huyo wa al-Shabaab kwamba asingemlazimisha binti yake kuolewa naye pasipo hiari yake. Hili lilimkasirisha mwanamgambo huyo, ambaye wakati huo alipata kibali cha kumkamata Ahmed kutoka katika mahakama ya al-Shabaab huko Elasha Biyaha, kitongoji cha Mogadishu.


"Siku moja baada ya kumwambia kwamba nisingeweza kumlazimisha binti yangu kuolewa na mwanaume asiyemtaka, aliniletea taarifa inayoniagiza kuripoti mahakamani ndani ya saa 24," Ahmed alisema.

Kukataa kumuozesha binti yake kwa mpiganaji ilikuwa ni dhambi, mahakama ilimwambia. "Nililazimishwa kumuozesha msichana kwa mwanaume palepale mahakamani," alisema. "Niliambiwa kumkabidhi msichana kwa mume wake ndani ya siku tatu; Sikupewa fursa ya kushauriana na mama wa msichana kuhusu ndoa."

"Baada ya kumueleza mama ya Zamzam kuhusu ndoa ya kulazimisha, tulianza kuchangisha fedha kutoka kwa ndugu na siku mbili baadaye, mke wangu, Zamzam na wadogo zake wa kike wawili walikimbilia Uganda," alisema.

Lakini al-Shabaab walipogundua kwamba wametoroka, wanamgambo walimkamata tena Ahmed.

"Nilihukumiwa bila ya kufuata haki kutumikia kifungo cha miezi sita jela, ambacho nilikimaliza mwaka 2010, lakini namshukuru Mungu mabinti zangu waliepukana na mateso ya kuwa wake za magaidi," alisema, akiongeza kwamba mahakama iliamuru mpiganaji wa al-Shabaab kumpa talaka Zamzam.

Familia ya Ahmed ilirejea Somalia mwaka 2013 na sasa wanaishi kwa amani katika wilaya ya Hodan huko Mogadishu.

"Mimi na familia yangu tuna furaha kuhusu kushindwa kwa al-Shabaab," alisema, akililaumu kundi hilo kwa "kuwafanya watu kukaribia kuichukia nchi yao wenyewe" kwa sababu ya unyanyasaji ambao ilibidi waupitie chini ya utawala wa al-Shabaab.

Mkaazi mwingine wa Mogadishu, Sadiyo Mumin mwenye umri wa miaka 55, alieleza ni jinsi mji ulipokuwa chini ya udhibiti wa al-Shabaab alivyoogopa mabinti zake wawili watalazimishwa kuolewa na al-Shabaab. Aliwapeleka mabinti zake -- ambao wakati huo walikuwa na miaka 19 na 22 -- kuishi na ndugu huko Ethiopia. Mumin mwaka huu alimrejesha binti yake nyumbani kwao wilaya ya Hodan.

"Shukrani zote kwa Mungu kwa kuwaondoa al-Shabaab na kuwaokoa mabinti zetu," aliiambia Sabahi. "Hatuna hofu tena ya al-Shabaab kulazimisha kuwaoa mabinti zetu kwa sababu wamesambaratika na kupata laana [ziwe juu yao] kwa mateso yote waliyoyasababisha."

Shamso Ali, mkaazi wa Daynile, mwenye umri wa miaka 26, ni bibi wa aliyekuwa mwanachama wa al-Shabaab. Kwa miaka mitatu, alikuwa katika ndoa na mwanachama wa al-Shabaab bila ridhaa yake, mpaka alipokufa katika mapigano na vikosi vya wanajeshi wa serikali mwaka 2012.

"Wakati alipokuwa ananioa, aliniambia atamwambia baba yangu kwamba tulitaka kuoana na [alinitishia] angemuua baba yangu pamoja na mimi kama ningekataa," alisema. "Nilisikitika sana na kuwa na hofu na nilikuwa naogopa kwamba baba yangu angeuawa kama ningelitoroka jiji".

"Hatukuwa na njia ya kupata fedha kwa ajili yangu wala wanafamilia wengine kutoroka, hivyo niliamua kukubali pendekezo hili kabla [hali hiyo] haijaenea," alisema. "Ninamshukuru Mungu kwamba maisha ya giza niliyoshirikiana na mtu niliyekuwa namwogopa hayapo tena na kwamba sikumzalia watoto."

Ndoa za kulazimishwa 'hazina msingi katika Uislamu'
Kama ilivyokuwa kwa Ali, wasichana wengine wengi ambao walilazimishwa kuolewa na wanachama wa al-Shabaab waliishia kuhangaika katika maisha kama wazazi pekee wa kike, wanaotakiwa kutafuta mahitaji kwa ajili ya watoto wao bila kuwa na msaada wa baba zao ambao waliwatelekeza kwa kuenda vitani bila kuwapa fedha yoyote.

Aina hii ya ndoa hakiubaliki kisheria katika Uislamu bila kujali nani anayehusika, kwa mujibu wa Sheikh Nur Barud Gurhan, mtumishi maarufu wa dini wa Kisomali na msemaji mkuu wa Umoja wa Wanazuoni wa Kiislamu nchini Somalia.

Alisema al-Shabaab walianza kutumia mbinu hii chini ya mwavuli wa Uislamu tangu mwaka 2007, wakitumia fursa ya familia maskini za Kisomali ambazo tayari zimezidiwa na hali ya matatizo na vita ambavyo vilikuwa vinaikabili nchi hiyo kwa miaka mingi.

"Waliwachukua wanawake wengi, wakiwalazimisha kuolewa na kuwanyanyasa ili kuwafanya wafikiri kuwa wasingeweza kumkataa kisheria mujahidina anayepigana [kulinda] dini na nchi," aliiambia Sabahi, akiongeza kwamba wanawake na familia ambazo walikaidi walikabiliwa na adhabu za kikatili kutoka kwa kundi hilo.

Ushahidi kwamba malengo ya al-Shabaab hayakuwa kuendeleza ndoa za kudumu au kuanzisha jamii yenye utulivu, wanamgambo hao pia waliwaoza wanawake wasio wenyeji wa Somalia kwa wapiganaji wa kigeni ambao walikuwa hawazungumzi Kisomali, wakijua hawatakuwa na uwezo wa kuwasiliana nao au kuwa na uhusiano na wake zao katika njia yoyote ya kueleweka.

"Ndoa kama hiyo hairuhusiwi kisheria katika Uislamu; haina uzuri wowote zaidi ya kubaka na hakuna msingi kama huo katika Uislamu," mtumishi huyo wa dini alisema.

Chanzo: http://sabahionline.com/

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top