Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This
Hatimaye kile ambacho kimekuwa kinakwepwa kwa miaka mingi juu ya mfumo wa Muungano wa Tanzania ambao mbali ya kuwa donda ndugu na kugharimu nafasi za wanasiasa wengi sasa kimepata utatuzi baada ya Tume ya Katiba Mpya kutoa pendekezo la kuundwa kwa Muungano wa serikali tatu.

Akiwasilisha Rasimu ya Katiba Mpya jana, Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba, alisema baada ya kujadiliana kwa kina katika kuchambua maoni ya wananchi juu ya mfumo wa Muungano unaofaa, Tume imefikia uamuzi wa kupendekeza serikali tatu, ya Shirikisho, Tanzania Bara na ya Zanzibar.


Jaji Warioba alisema kazi ya kufikia uamuzi huo haikuwa rahisi kwa sababu katika maoni mbalimbali yaliyotolewa na wananchi, wapo waliokuwa wanataka Muungano wa serikali moja, serikali nne, kuendelea na muundo wa sasa wa serikali mbili na pia walikuwako wa Muungano wa mkataba.


“Kimsingi sheria ilitutaka kuzingatia uwapo wa Muungano. Kwa hiyo hatukuchukua maoni ambayo yanataka kuvunja Muungano ingawa yalikuwapo ya watu wachache,” alisema katika rasimu aliyowasilisha kwa umahiri mkubwa na kuonyesha kugusa maeneo mengi ambayo yanakidhi kiu ya wananchi wengi.


Alisema kabla ya kufikia uamuzi huo, walifanya rejea ya mapendekezo na maandiko mbalimbali, kutazama uzoefu wa mataifa mengine, lakini pia kuzingatia mapendekezo ya Tume ya Jaji Francis Nyalali na Jaji Robert Kisanga.


Tume zote zilipendekeza kuwapo kwa Muungano wa serikali tatu.


Katika kushughulikia Muungano, Jaji Warioba pia alisema kuwa orodha ya mambo ya Muungano yamepunguzwa kutoka 22 hadi saba.


Aliorodhesha mambo saba ya Muungano ambayo ndiyo yatapelekwa kwa wananchi ili kutolewa maamuzi, kuwa ni Katiba, Ulinzi na Usalama, Uraia na Uhamiaji, Sarafu na Benki Kuu, Mambo ya Nje, Usajili wa Vyama vya Siasa, Ushuru wa Bidhaa na Mapato yasiyokuwa ya kodi.


Katika mapendekezo hayo ya kihistoria, pia muundo wa Bunge la Muungano nao umeguswa na sasa litakuwa na viti 75 tu, kwa uwiano wa wabunge kutoka Tanzania Bara 50 na Zanzibar 20, huku wabunge watano wakiwa ni wa kuteuliwa na Rais kutoka kundi la walemavu.


Rasimu hii mpya ambayo itakuwa na ibara 240 kuliko ilivyo sasa yenye ibara 152, inafuta wabunge wa viti maalum, na badala yake kila jimbo la uchaguzi litakuwa na wabunge wawili, mmoja mwanamume na mwingine mwanamke, hali ambayo itasaidia kuleta usawa wa kijinsia.


Kwa maana hiyo, kama mapendekezo hayo yatakubaliwa na wananchi kupitia kura ya maoni, Tanzania Bara itakuwa na majimbo ya uchaguzi 25 wakati Zanzibar itakuwa na majimbo 10 tu.


Kwa sasa Tanzania Bara ina majimbo ya uchaguzi 189 wakati Zanzibar ni 50 ikifanya jumla ya majimbo yote kuwa 239. Pia Rais ana nafasi 10 za wabunge wa kuteuliwa.


Katika kudhibiti nafasi za ubunge na kukuza uwajibikaji, Tume inapendekeza wananchi kuwa na haki ya kumwita mbunge na kumuhoji ikibidi kumwondoa kwenye nafasi yake, kitu ambacho mfumo wa sasa hauna kwani akishachaguliwa hukaa hadi kipindi chake cha miaka mitano kimalizike hata kama hafanyi lolote.


Udhibiti wa ubunge pia umekwenda kwenye pendekezo la kuwa na ukomo wa ubunge ambao ni miaka 15 ambayo mtu hataruhusiwa tena kugombea.


Tume inapendekeza kufutwa kwa mfumo wa uchaguzi mdogo na badala yake lolote litakalotokea kwa mbunge wa jimbo anayetokana na chama cha siasa kama ataondolewa, basi orodha ya wanachama wengine wa chama hicho itakayowasilishwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi ambayo itatueua mmoja kwenye orodha hiyo kuziba nafasi hiyo kutoka chama kilichopoteza mbunge.


Hata hivyo, Tume inapendekeza kuwa uchaguzi mdogo utafanyika tu endapo mbunge aliyepoteza nafasi yake ni mgombea binafsi.


MGOMBEA BINAFSI RUKSA

Kwa maana hiyo, Tume inapendekeza mfumo wa mgombea binafsi kuanzia ngazi ya mwenyekiti wa mtaa hadi nafasi ya rais.

Suala la mgombea binafsi limekuwa ni moja ya maeneo ambayo yamezua mvutano nchini kwa serikali kupambana kufa kupona kuzuia kuwako kwa fursa hiyo.


Serikali ilikwisha kushindwa kesi mara mbili juu ya mgombea binafsi, lakini ikapambana kwanza kwa kutunga sheria ya kuharamisha mgombea binafsi, lakini baadaye kwa kuomba rejea ya kesi Mahakama ya Rufaa dhidi ya hukumu iliyohalalisha fursa hiyo. Kesi hiyo kwa sasa iko katika Mahakama ya Afrika mjini Arusha.


SPIKA NA NAIBU SPIKA

Katika rasimu hiyo, Tume pia inapendekaza kuwa Spika na Naibu wake wasiwe wabunge na wala wasiwe viongozi katika vyama vya siasa.

Katika siku za hivi karibuni kiti cha Spika kimekuwa kikilaumiwa kuyumba kupendelea chama anachotokana nacho, hali ambayo imelifanya Bunge kukosa usawa kwa pande zote, yaani upande wa chama tawala na ule wa upinzani.


TUME HURU YA UCHAGUZI

Tume hiyo pia inapendekeza kuundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi ambayo pia itachukua majukumu ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

Rasimu inapendekeza wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi wapatikane kwa kuzingatia sifa ambazo zitaanishwa kwenye katiba, na wanaohitaji nafasi hizo wataomba kwa Kamati ya Uteuzi ambayo itaongozwa na Jaji Mkuu, majaji wakuu kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, Maspika kutoka pande mbili za Tanzania- Baraza la Wawakilishi na Bunge na Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.


Aidha, Tume inapendeleza kuwa baada ya mchakato huo, Rais akishateua Mwenyekiti wake jina litawasilishwa bungeni ili kuthibitishwa.


MAHAKAMA

Tume inapendekea kuendelea na mfumo wa sasa wa kuzingatia uhuru wa mahakama, lakini inapendeleza pia kuanzishwa kwa Mahakama ya Juu (Sprime Court of Tanzania).

Pia ipendeleza kuwa huduma zaidi kwa maana ya rasilimali zitolewa kwa mahakama ili itekeleze kazi zake kwa uhuru na haraka zaidi.


MADARAKA YA RAIS

Tume inapendekeza kuendelea kuwa na Rais mtendaji ambaye anachaguliwa na wananchi kwa kura katika uchaguzi mkuu.

Pia ashinde kiti cha urais baada ya kupata kura zaidi ya asilimia 50 ya kura zote badala ya utaratibu wa sasa wa kuwazidi wenzake kura hata kama siyo kufikia kiasi kinachopendekezwa.


Rais anapendekezwa kuendelea kuwa Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama; na sifa za sasa kugombea urais kwa mujibu wa katiba ziendelee ikiwa ni pamoja na umri uwe ni kuanzia miaka 40.


Matokeo ya uchaguzi urais sasa itakuwa ni ruksa kuhojiwa mahakamani katika Mahakama ya Juu na ni lazima shauri hilo liwe limesikilizwa na kufanyiwa uamuzi katika kipindi cha siku 30 ili Rais mpya aapishwe ndani ya muda unaokubalika kikatiba.


Hata hivyo, anayetakiwa kisheria kuhoji matokeo hayo ni aliyegombea kiti hicho.


MADARAKA YA RAIS YAPUNGUZWA

Tume inapendekeza kuanzishwa kwa utaratibu wa wateule wa rais kuthibitishwa na bunge, kuteuliwa kupitia mchakato wa taasisi na vyombo vingine katika uteuzi. Kwa sasa ni Waziri Mkuu pekee anayethibitishwa na Bunge.

Imependekezwa kuwa uteuzi wa mawaziri, manaibu mawaziri, jaji mkuu, naibu jaji mkuu utafanywa na Rais na Bunge kuwathibitisha.


Hata hivyo, jaji mkuu na naibu wake watateuliwa na Rais kutokana na majina yatakayopendekezwa na Tume ya Utumishi wa Mahakama.


Wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama wapitishwe na Baraza la Ulinzi na Usalama; Katibu Mkuu Kiongozi ateuliwe na Rais, lakini athibitishwe na Bunge; makatibu wakuu wateuliwe na Tume ya Utumishi wa Umma; mawaziri na manaibu wao wathibitishwe na Bunge.


Kinga dhidi ya Rais endelee kama ilivyo, isipokuwa kama Bunge litaamua linaweza kuanzisha mashitaka dhidi ya Rais kama inavyofafanuliwa kwenye katiba ya sasa.


MAWAZIRI WAPUNGUZWA

Tume inapendeleza Katiba iweke ukomo wa idadi ya mawaziri ambayo itakuwa ni 15 kwa kuwa tayari majukumu mengi yatakuwa yamekwisha elekezwa kwenye serikali Tanzania Bara na Zanzibar.

CHANZO: NIPASHE

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top