Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad amewataka Wanachama na Wazanzibari kwa Ujumla kuendelea kushikamana katika kipindi hiki cha kuitolea Maoni Rasimu ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ili lengo la Zanzibar kuwa na Mamlaka yake kamili liweze kufikiwa.

1
Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad akiwahutubia wafuasi wa chama hicho katika mkutano wa hadhara uliofanyika Matemwe, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Amesema mshikamano ndio uliosaidia Rasimu hiyo kupunguza mambo ya Muungano kutoka 22 hadi 7 na kwamba jitihada zinapaswa ziendelee katika kujenga hoja ili Wizara ya Mambo ya Nje, Benk Kuu na Sarafu, Vyama vya Siasa, Uraia na Ushuru wa Bidhaa kutolewa katika Mambo ya Muungano.

Maalim Seif amesema hayo wakati akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika Matemwe, Mkoa wa Kaskazini Unguja mwishoni mwa wiki.

Amesema kwa maoni yake Tume ya mabadiliko ya katiba imefanya kazi kubwa ya kukusanya na kuchambua maoni ya wananchi na hatimaye kupata rasimu ya awali ya katiba ambayo imezingatia baadhi ya matakwa ya wazanzibari.

Amesema pamoja na mambo mengine rasimu hiyo ya awali imezingatia kwa makini uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imeundwa na nchi mbili yaani Zanzibar na Tanzania Bara na kwamba mara kwa mara Rasimu hiyo imekuwa ikitaja washirika wa Muungano.


Mambo mengine aliyoeleza kuyakubali katika rasimu hiyo ni pamoja na kutamka wazi kuwa masuala ya Mafuta na gesi asilia, Mikopo na biashara za nje, Ushuru wa forodha, pamoja na elimu ya juu na baraza la mitihani kutokuwa katika Orodha ya Mambo ya Muungano.

Hata hivyo amesema kuna mambo kadhaa yanayohitajika kurekebishwa katika rasimu hiyo ili kufikia lengo la kuwa na Zanzibar yenye mamlaka kamili.

Ameyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na jina la Muungano ambao kwa maoni yake unapaswa kuitwa “Muungano wa Jamhuri za Tanzania”, tofauti na ilivyo sasa “Jamhuri ya Muungano wa Tanzania”.

Mambo mengine aliyoeleza kutoridhishwa nayo kwenye rasimu hiyo ni pamoja na Mambo ya nje kubakia katika orodha ya mambo ya Muungano, sarafu na benki kuu, uraia na uhamiaji pamoja na vyama vya siasa.

“Tunataka Zanzibar iwe na uwezo wa kufanya mambo yake bila ya kuingiliwa, kwa mfano iwe na uwezo wa kujiunga na Umoja wa Mataifa (UN), Umoja wa Afrika (AU), pamoja na FIFA”, alieleza Maalim Seif.

Aidha amesema baadhi ya vipengele vya rasimu hiyo havikutolewa maelezo ya kutosha, hali inayowafanya wananchi kutoelewa mantiki halisi iliyokusudiwa, na kuiomba tume ya Mabadiliko ya Katiba kuvitolea ufafanuzi.

Miongoni mwa vipengele hivyo ni Muundo wa Muungano ambapo amesema zilizoungana tangu asili ni Tanganyika na Zanzibar, na kutaka Tume iweke wazi washirika hao wa Muungano.

Hata hivyo amesema rasimu hiyo bado ina kasoro nyingi ambazo zinapaswa kujadiliwa zaidi katika mabaraza ya katiba, ili kupata rasimu ya pili itakayokidhi matakwa ya wananchi, kabla ya rasimu hiyo kufikishwa katika Bunge la katiba.

Maalim Seif amefahamisha kuwa Chama cha Wananchi CUF kimeunda jopo la wataalamu wa Sheria kwa ajili ya kuipitia na kuichambua rasimu ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyotolewa hivi karibuni.

Amesema jopo hilo la wataalamu litakapokamilisha kazi yake, litakuwa na upeo mkubwa wa kuushauri uongozi wa chama hicho, ili kiweze kutoa tamko rasmi la Chama kuhusiana na rasimu hiyo ya katiba.

Amesema bado wananchi wana fursa ya kuchangia katika rasimu hiyo kupitia wawakilishi wao watakaoingia katika mabaraza ya katiba ambapo wananchi watatoa uamuzi wa mwisho wakati wa kura ya maoni.

Wakati huo huo Maalim Seif amewatahadharisha wananchi kutojihusisha na vitendo vyovyote vya vurugu na uvunjifu wa amani katika kuendelea na mchakato huo.

Kabla ya mkutano huo, Maalim Seif alifungua baraza ya CUF ijulikanayo kwa jina la “msimamo” au “mtendeni Namba 2” katika kijiji cha Mfurumatonga, yenye wanachama 200.

Kwenye mkutano wa hadhara alikabidhi kadi za CUF 609 kwa wanachama wapya walioamua kujiunga na chama hicho, huku 148 kati yao wakiwa wamerejesha kadi za CCM.

Naye Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa CUF Taifa Salim Bimani, aliwakumbusha wananchi kujisajili katika daftari la kudumu la wapiga kura muda utakapofika.

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top