Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This


Alex Ferguson
Kocha wa Manchester United anayestaafu Alex Ferguson Mei 12, 2013.
Sir Alex Ferguson aliyetangaza kustaafu mwishoni mwa msimu huu ataingia katika mabuku ya kumbukumbu kwa kujizolea sifa kochochoko katika taaluma yake ya ukufunzi kwa kipindi cha miaka 26 akinoa Manchester United.

SIR Alexander Chapman Ferguson 'Fergie’ aliyetangaza kustaafu mwishoni mwa msimu huu ataingia katika mabuku ya kumbukumbu kwa kujizolea sifa kochochoko katika taaluma yake ya ukufunzi kwa kipindi cha miaka 26, akiinoa klabu moja; Manchester United!
Sio sifa tu bali pia fedha alizojikusanyia kwa kipindi hicho zilimweka miongoni mwa makocha matajiri duniani.MAISHA YAKE BINAFSIFerguson aliyezaliwa Desemba 31, 1941 alimwoa mkewe Lady Cathy Holding 1966.Wawili hao walijaliwa watoto watatu Mark 45, Darren na Jason 41 ambao ni mapacha.
Darren aliwahi kuchezea kikosi cha Manchester United miaka ya tisini kabla ya kufuata nyayo za babake za ukufunzi. Kwa sasa anainoa klabu ya Peterborough United.

FEDHA
Kwa mujibu wa orodha ya Sunday Times Sport Rich List 2013, Fergie ndiye kocha tajiri nchini Uingereza akikadiriwa kuwa na utajiri wa Sh4.4 bilioni huku akipokea ujira wa Sh858 milioni kila mwaka.
Roy Keane mchezaji wake wa zamani, sasa akiwa mkufunzi anafuata orodha hiyo kwa Sh3.8 bilioni.
 Arsene Wenger pia yuko katika nafasi hiyo huku Roberto Mancini akitamatisha nne bora kwa Sh2.7 bilioni. Duniani, anaorodheshwa katika nafasi ya tatu miongoni mwa makocha wanaolipwa mshahara mkubwa, Jose Mourihno anaongoza kwa Sh1.3 bilioni, Mancini akiwa katika nafasi ya pili kwa Sh975, Wenger akiwa wa nne kwa Sh780 milioni naye Carlo Ancelotti akihitimisha tano bora kwa Sh650 milioni.
Utajiri wa Ferguson unasemakana kuwa nusu ya ule wa dereva mashuhuri wa langalanga, Lewis Hamiliton anayeorodheshwa wa tatu miongoni mwa madereva matajiri wa langalanga duniani akimiliki Sh7.8 bilioni.

MAJUMBA
Fergie anamiliki jumba la kifahari lililojengwa kwa kipande cha ardhi cha ekari 1.5 jijini Macclesfeild, Uingereza. Analo jumba jingine mjini Wilmslow, Cheshire anakoishi na mkewe Cathy.

MAGARI
Licha ya kuwa mkwasi, kocha huyu hajaonekana kuvutiwa sana na umiliki wa magari mengi ya kifahari kama nyota wengi wa soka. Ferguson amewahi kunukuliwa akisema kuwa hapendi kuendesha magari sana kwa kuwa huhofia usalama wake, huenda ikiwa ndio sababu ya yeye kutopenda magari.
Hata hivyo, magari mawili ya kifahari yanayojulikana kuwa yake ni Audi A8 lililomgharimu Sh11 milioni na Chevrolet Volt lenye gharama ya Sh4.6 miloni. Gari hilo hutumia nguvu za umeme baada ya kutiwa chaji kwa masaa 24. Pia hutumia petroli hasa chaji inapokwisha.

UWEKEZAJI
Tajriba yake ya miaka mingi kama meneja wa klabu kubwa inayozoa faida ya mamilioni ya pesa kila mwaka ilimpa maarifa mengi ya uwekezaji. Utajiri wake hautokani tu na soka bali pia na biashara anazoendesha.
Yeye ni mwanachama na mshikadau katika kampuni za filamu za Eclipse 35, Clyde Films, Cherwell Films na Scotts Atlantic Partners. Pia anamiliki kampuni ya kibinafsi ya mchezo wa uendeshaji farasi, farasi wawili 'What A Friend’ na 'Harry The Viking’. Kampuni yake hujisajili kwenye mashindano kadha ya farasi kila mwaka.
MIGOGORO
Kutokana na msimamo wake mkali wa kiukufunzi na presha ya kuwa meneja wa klabu ya hadhi ya Manchester, ingekuwa vigumu kwa Fergie kutotofautiana na wengi kwa kuwakashifu, miongoni mwao ni wachezaji, shirikisho la soka la Uingereza, FA, makocha wenzake na hata baadhi ya marefa.
Kwa kipindi cha miaka 26, Fergie alikuwa amejihusisha na migogoro mingi, haya ni baadhi yayo atakayokumbukwa sana kwayo.
Mnamo 1997 kocha wa Arsenal, Arsene wenger alipojiunga na klabu hiyo ya Uingereza akitokea ile ya Nagoya Grampus nchini Japan, Fergie alimtaja kama limbukeni katika taaluma ya ukufunzi na akamtaka kila anapotoa maoni yake kuhusu hali ya soka nchini Uingereza, aelewe kwamba soka ya Uingereza sio sawa na ile ya Japan.
Hali hii ilizua chuki kubwa baina yao na hata kuchochewa zaidi na ushindani mkali baina ya timu zao.
Miaka 10 baadaye, uhasama huo ulififia hasa Arsenal ilipoanza kupata matokeo duni na kupunguza ushindani. Mwaka 2004, Fergie aliapa kutozungumza kamwe na shirika la habari la BBC baada ya chombo hicho cha habari kuangaza kipindi kilichomkashifu mwanawe Jason ambaye ni wakala wa kandanda.
Alitaja kipindi hicho kuwa cha uvumi mtupu uliolenga kumshusha hadhi mwanawe.
Desemba mwaka huo, kocha huyo alisema kuwa hawezi kuiuzia klabu ya Real Madrid ya Uhispania chochote hata kama ni 'virusi’ ila kufikia Juni mwaka huo alikubali kuuza David Beckham kwa klabu hiyo na baadaye kuwauza wachezaji wengine mahari akiwemo Cristiano Ronaldo, Rud van Nestroy na Gabriel Heinz.
Zaidi ya Wenger, amezozana na wakufunzi wengine kama Sam Allaydace, Allan Pardew (alipotaja klabu yake ya Newcastle United kama duni). Chuki yake na Rafael Benitez wa Chelsea ilidumu kwa zaidi ya muongo mmoja.
Benitez alipokuwa akiinoa Liverpool hadi 2010, alimkashifu Ferguson kwa kuandaa orodha ya mambo 10 kumhusu Ferguson hasa akimtaja kama mtu mwenye majitapo anayejiona kujua kila kitu. Fergie aliyapuuza na kumtaja Benitez kama mpuuzi.
Mchezaji aliyewahi tofautiana vibaya sana na kocha huyu kwenye taaluma yake ni Beckham. Beckham alimjibiza vibaya kocha huyo kwenye chumba cha wachezaji, naye kocha huyu akamtandika usoni na daluga.
Baadaye Fergie alimkashifu kwenye vyombo vya habari kwa kusema kuwa mchezaji huyo alibadili tabia baada ya kumwoa mkewe Victoria ambaye ni mwanasana.
Beckham aliuzwa baadaye kufuatia tofauti hiyo.
FA imemtoza faini ya mamilioni ya pesa na pia kumpiga marufuku ya kuhudhuria baadhi ya mechi, zaidi ya mara saba kwa kuwakashifu wasimamizi wa michuano mbalimbali.
Aidha, kukashifu usimamizi wa shirikisho hilo umemtia matatani.
Pia amekuwa na cheche za maneno kwa klabu ya Manchester City, majirani na mahasimu wao. Baada ya klabu hiyo kufaulu kumshawishi straika Carlos Tevez kujiunga nayo kutoka Man United, kocha huyo ambaye alitaka sana kusalia na mchezaji huyo aliisuta klabu hiyo kwa kusema kuwa kumchukua mchezaji huyo hakungeathiri klabu yake kwa vyovyote na City haipaswi kujigamba sana kwani ni klabu ndogo wala haiwezi kuifikia hadhi ya United.

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala,

Hifadhi blog hii kwenye simu yako ili upate habari zote kwa urahisi zaidi

Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro
http://www.facebook.com/kibonajoro

Post a Comment

 
Top