
KIUNGO mwenye kasi, Mrisho Khalfan Ngassa, amerejea Yanga na kusaini mkataba wa miaka miwili kuichezea tena timu hiyo. Ngassa
alianza kupata umaarufu mkubwa akiwa na Yanga kabla ya kuondoka na
kujiunga na Azam FC kwa kitita cha jumla ya Sh milioni 98 na kuweka
rekodi mpya ya usajili. Lakini
Ngassa ameamua kusaini tena mkataba wake mpya Yanga wakati akiwa chini
ya klabu ya Simba ambao ni watani wakubwa wa Yanga.
Simba
na Yanga zinakutana Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam
katika mchezo wa mwisho kufunga msimu, huku Yanga wakiwa wamepania
kulipa kisasi cha mabao 5-0.
Mechi
hiyo ndiyo itakuwa ya mwisho kwa Ngassa ambaye mkataba wake umesainiwa
bila kuwa na tarehe, Championi Jumatano limeshuhudia na lina uhakika
asilimia mia.
“Mkataba na Ngassa kila kitu kimekamilika kama unavyoona, hapa
tunachosubiri ni kuisha kwa msimu na mara moja atatua na kuanza kazi
Jangwani,” alisema mmoja wa viongozi ambao huhusika na masuala ya
usajili Yanga.
Alipoulizwa kwa nini mkataba huo ambao una saini ya Ngassa na dole gumba
lake hauna tarehe, alijibu: “Bado hatujajua utaratibu wa TFF kama
mkataba ukisainiwa kabla ya mwingine kuisha inakuwaje. Hatutaki kuingia
kwenye matatizo na mtu.
“Kitu kizuri Ngassa baada ya mkataba wake na Azam FC kuisha, sasa ameamua kurudi nyumbani, nasi tumemkaribisha vizuri.”
Ingawa mhusika alifanya juhudi za kuficha eneo la malipo ya Ngassa
lakini taarifa za uhakika zinaonyesha atakuwa analipwa dola 2000 (Sh
milioni 3.2) kwa mwezi.
Kwa mshahara, Ngassa atakuwa mchezaji anayelipwa zaidi ya wachezaji wote
Ligi Kuu Bara. Labda kama kuna timu kati ya Yanga, Simba au Azam FC
itasajili mwingine na kumpa zaidi ya hizo.
Kwa misimu miwili Felix Sunzu amekuwa akiongoza. Analipwa dola 3,500 (Sh
milioni 5.6), Mzambia huyo amemaliza mkataba na Simba, ataondoka.
Wakati Ngassa akiwa Azam na Simba alikuwa anachukua Sh milioni 2 kwa
mwezi.
Kuhusiana na fedha za usajili, kwa kuwa Ngassa ametua Yanga kama
mchezaji huru, tayari ameshatanguliziwa ‘kishika uchumba’ cha Sh milioni
10 pamoja na gari aina ya Nissan Trail ambalo thamani yake inafikia
hadi Sh milioni 23.
Ngassa amekuwa akilitumia gari hilo alilopewa na Yanga baada ya kuuza
alilopewa na Simba aina ya Toyota Verrosa lenye thamani ya Sh milioni 16
kwa hofu ya kupokonywa na Simba siku atakaposema anakwenda Yanga.
Kuna taarifa kuwa Ngassa alisaini mkataba mwingine na Simba ambao angeanza kuutumikia baada ya mechi hiyo ya Jumamosi.
Simba kupitia kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Zacharia Hans Pope,
imetangaza kwamba Ngassa alisaini mkataba mwingine wa mwaka mmoja,
akapewa gari na fedha Sh milioni 30 na kama anataka kwenda kokote, basi
atalazimika kurudisha fedha hizo.
Lakini Ngassa amekuwa akisisitiza hana mkataba na Simba na baada ya huo
wa Azam FC iliyompeleka Simba kwa mkopo utakapomalizika, atakuwa huru
kwenda anakotaka.
Ngassa ambaye yuko kambini na Simba mjini Zanzibar, amewahi kuliambia
Championi kwamba kama Simba inamtaka abaki, basi lazima itoe kitita cha
Sh milioni 150.
source:champion
Facebook Blogger Plugin by Kibonajoro







Post a Comment
Post a Comment